MAMLAKA
ya Chakula na Dawa (TFDA) kanda ya kati Dodoma juzi ileteketeza tani tatu za
madawa, chakula na vipodozi ambavyo havifai kwa matumizi ya binadamu ambapo
bidhaa zote zikiwa na thamani ya Sh. Milioni 19.
Katika
hali ya kustaajabisha baadhi ya wakazi wanaoishi karibu na eneo la dampo la
Mbwanga ambao walikusanyika kushuhudia tukio la kuteketezwa kwa
bidhaa hizo walikuwa wakiomba wapatiwe bidhaa hizo ili waweze kuzitumia na hata
kuziuza.
Baadhi
ya wananchi hao ambao waliweka mikono kichwani kusikitika bidhaa hizo zikiteketezwa
mbele yao walisema wako tayari kudhurika kuliko kuona pipi, blueband, maziwa ya
kopo yakiteketezwa mbele yao ni heri wangepewa ili wakatumie..
Miongoni
mwa bidhaa zilizoteketezwa ni masanduku 20 ya soda ambazo zilikamatwa kwenye
moja ya maduka katika stendi kuu ya Dodoma ambazo zilikuwa kwenye friji.
Soda
hizo zilikuwa zimeisha muda wake lakini walikuwa wakiuziwa wateja wa mabasi
yanayosimama stendi ya Dodoma kitu ambacho wataalam wa TFDA wamesema ni hatari
na kutaka abiria kuwa makini pindi wanaposafiri kwani kununua bidhaa kwa haraka
wakiwa madirishani si salama kwa afya zao.
Kwa
mujibu wa Kaimu Meneja wa TFDA Kanda ya Kati, Florent Kyomo alisema zoezi hilo
litakuwa endelevu kwa lengo la kuondoa bidhaa sokoni bidhaa zisizofaa kwa
matumizi ya binadamu.
Alisema
mamlaka hiyo iwe macho na wataendelea kukagua na hata baadhi ya
wafanyabiashara waliowahi kukamatwa sasa wameamua kubadilika.
Kwa
upande wake Mkaguzi wa dawa wa TFDA, Dk.Engelbert Bilashoboke alisema
kuna baadhi ya maduka ambayo yanauza dawa ambazo hazifai kwa matumizi ya
binadamu hali inayopelekea mtumiaji kutumia dawa ambazo haziwezi kuponya
magonjwa yake.
Alisema
mnunuzi anaweza kuona amenunua dawa kumbe hata kile kilichoandikwa juu ya dawa
si kile kilichomo ndani yake.
“Unaweza
kuona ni dawa kumbe si dawa sahihi” alisema
Mkaguzi
wa Chakula wa Mamlaka hiyo, Sifa Chamgenzi alisema madhara ya kula vyakula
ambavyo havifai kwa matumizi ya binadamu ni makubwa.
“Unaponunua
chakula unatumaini kitajenga na kuupa mwili nguvu lakini chakula kinapokuwa
kwa ajili ya kuleta madhara kwenye mwili hili linakuwa ni tatizo kubwa.
Alisema
wanajitahidi kuelimisha watu waangalie vyakula vinavyofaa kabla ya kuvitumia
kwa kuona muda wa kutengenezwa na muda wa mwisho wa matumizi yya vyakula hivyo
”alisema
Miongoni
mwa bidhaa zilizoteketezwa ni pamoja na madawa ya binadamu, maziwa ya kopo,
blue band, Tomato sauce, Soda, pipi, sabuni za kuoshea sehemu za siri za
wanawake aina ya Kaisiki, sabuni za aina mbalimbali za kuondoa harara na upele,
madawa ya Kichina kwa ajili ya kuchua na mafuta ya kupikia.