Tuesday, March 11, 2014

Polisi yawashikilia wanane Dodoma



JESHI la Polisi Mkoani Dodoma linawashikilia watu wanane kwa kukutwa
na madawa ya kulevya aina ya bangi na mirungi pamoja na zana za
kufanyia uhalifu.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa
Polisi (SACP) David Misime alisema kukamatwa kwa watu hao kunatokana
na msako unaoendelea wa kupambana na wahalifu na uhalifu uliofanyika
eneo la Chang'ombe Machi 11, mwaka huu.
 
kamanda misime
Katika msako huo Polisi waliwakamata watuhumiwa hao wakiwa na kilo
moja na  misokoto 104 ya bangi, mirungi gram 500  zana za kuvunjia
yakiwemo mapanga, mikasi, visu na nondo.
Kwa mujibu wa Kamanda Misime msako huo ulihusisha zaidi kero za
uvutaji wa bangi na kupelekea kufanya uhalifu katika maeneo
mbalimbali Manispaa ya Dodoma.
Aliwataja waliokamatwa kuwa ni Halfan Muheza (25), Stewart Sylvester
(18), Shaban Ibrahim (18), Abdallah Idd (18), Fikiri Jonas (20), Ally
Nuru (30), Saimon Zabron (43) na Albert Charles (18)  wote wakazi
Chang'ombe Manispaa ya Dodoma.
Kamanda Misime alisema watuhumiwa wote watafikishwa mahakamani leo
kujibu tuhuma zinazowakabili.
Pia alisema Jeshi la Polisi linaendelea kumtafuta Dereva wa gari
linalosemekana kuwa ni Toyota Land Cruiser GX Standard rangi nyeupe
baada ya kumgonga mpanda baiskeli aliyefahamika kwa jina la Julias
Sanduku (50) Mkazi wa Gairo katika eneo la Kijiji cha Visimi Kibaigwa
na kumsababishia kifo mpanda baiskeli huyo.
Alisema dereva huyo alikuwa akitokea Dodoma kuelekea Morogoro baada ya
kumgonga mpanda baiskeli,alishuka kutoka ndani ya gari na kumwangalia
aliyemgonga alipogundua amefariki akageuza gari kurudi njia ya Dodoma
na kuwaambia wananchi waliojitokeza kuwa anaenda kutoa taarifa jambo
ambalo hakufanya.
 Kamanda Misime aliwaomba wananchi wenye taarifa na dereva huyo alipo
wajulishe katika kituo chochote cha Polisi ili aweze kukamatwa.

No comments:

Post a Comment