Tuesday, April 22, 2014

Mila ya kuondoa mikosi 'kitigo' ilivyomsababishia Ukimwi

“NILIPATA maambukizi ya Ukimwi mwaka 1990, nakumbuka baada ya kifo cha  mume wangu niliambiwa nirithiwe na mdogo wa mume jambo hilo nililipinga , nduguze wakasema kama sitaki kuolewa lazima uondoe kitigo (mkosi) bila hivyo utaua ukoo mzima huo ukawa ni mwanzo wa safari ndefu katika maisha yangu kwani baada ya muda mfupi nilianza
 kudhoofika na baadaye kugundulika ninaishi na VVU”

Maneno hayo yanasemwa na Rukia Issa Majata (59) mkazi wa Sahare Tanga.

 Nilimfahamu mwanamke huyu wakati wa kongamano la wanawake Kitaifa
 lililofanyika Mkoani Dodoma.Hata nilipomuomba kwa ajili ya kufanya
 naye mahojiano hakuwa na shaka.

“Mimi niko tayari wakati wowote na niko tayari kueleza kitu gani
 kimenitokea katika maisha yangu ili jamii izidi kuongeza juhudi
 kupinga mila potofu wanazofanyiwa wanawake na wakati mwingine zimekuwa
 zikigharimu maisha yao” anasema mama huyo.

 Akiwa ni mwanaharakati wa masuala ya Ukimwi na hata nyanja za ukatili
 wa kijinsia anasema kuwa, aliolewa mwaka 1972 na Denea Mwendo ambaye
 kwa sasa ni marehemu.

 Anasema kuwa,mume wake alifariki mwaka 1990 na wakati huo tayari
 alikuwa na watoto wanane.

 Hata hivyo,anasema kuwa,baada ya msiba huo kuisha wana ukoo walikaa na
 kuamua aridhiwe na mdogo wa mume wake jambo ambalo hakukubaliana nalo
 lakini wakasema kama hataki kurithiwa ni lazima aondoe kitigo (mkosi)
 la sivyo atamaliza ukoo mzima.

 Anasema kuwa  aliambiwa hayo kabla hata hajamaliza eda, japo alikuwa
 akikataa lakini alikuwa hana sauti kutokana na wao kuwa wengi na
 alitakiwa kutafutwa mwanaume aliyefiwa na mume ambaye alikuwa
 hamfahamu

 Ndipo ulipofika usiku akasindikizwa na mwanamke moja ambaye hamfahamu
 kwa jina na yule bwana wa kwenda kumuondoa kitigo alisindikizwa na
 mwanaume mwenzake na walipofika huko wakafanya tendo la ndoa huku wote
 wakiwa hawajuani,  wakati huo ilikuwa ni saa nne za usiku kwa hiyo
 ilikuwa si rahisi kumtambua mtu kutokana na giza lililokuwepo.

 Rukia anasema kuwa, baada ya miezi sita  akaona afya yake inashuka na
 wakati huo ilikuwa ni mwishoni mwa mwaka 1990 ,akaona ni heri akapate
 ushauri wa kupima virusi vya Ukimwi.

 Baada ya kupima akagundulika kuwa ana maambukizi ya Virusi vya Ukimwi
 hali ambayo ilimchanganya lakini akaamua kumshukuru Mungu kwa kila
 jambo.

 Hata hivyo alipewa rufaa ya kwenda hospitali ya Bombo kwa ajili ya
 kupima ini, wingi wa damu na CD4 na baada ya wiki moja alifuatilia
 majibu  na kuonekana kuwa alikuwa na CD4 1050 jambo ambalo lilifanye
 asianze kutumia dawa.

‘Nilipewa mlolongowa chakula ambachokitanisaidia na mambo ambayo
 yatafanya nisishushe kinga yangu”anasema

 Anasema kuwa mwanaume aliyemfanyia kitigo ndiye atakuwa amemuambukiza
 Ukimwi kwani hata marehemu mume wake hakuwahi kuugua ugonjwa huo na
 alianza kudhoofika muda mfupi baada ya kubakwa na mwanaume aliyetakiwa
 kumuondoa mkosi.

 Japokuwa aliamua kumuachia Mungu juu ya maisha yake na kuamua kuishia
 kwa masharti aliyokuwa akielekezwa na masdaktari hali ambayo imemfanya
 kuwa na afya njema mpaka sasa.

 Hata hivyo anasema kuwa, mwaka 2006 alifiwa na binti yake  aliyemtaja
 kwa jina la Rehema na hapo kinga yake ya mwili ikashuka kutokana na
 mshtuko ambao ulifanya ashindwe kula na wakati huo ndiyo alianza
 kutumia dawa za kupunguza makali ya Ukimwi (ARV).

 Anasema kuwa tangu wakati huo ameendelea kutumia ARV lakini mpaka sasa
 CD4 zake ziko1066.

 Siri ya mafanikio

 Rukia anasema kuwa,ameamua kuwa kioo cha jamii na amekuwa akielimisha
 vijana mashuleni na sehemu mbalimbali ikiwemo kwenye mikutano, warsha
 na makongamano endapo atachaguliwa kwani amekuwa hana wasiwasi kabisa.

“Mwaka 1999  nilijitangaza kuwa ninaishi na virusi vya Ukimwi  hiyo ni
 baada ya kujiunga na Umoja la watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi Mkoa
 wa Tanga TAPHA+  na baada ya kujitangaza baadhi ya watu waliamini na
 wengine hawakuamini lakini nilikuwa nimeondoa mnyororo wa wasiwasi”
anasema

 Anasema baada ya kujitangaza kuna watu walikuwa wakimnyooshea vidole
 lakini hakujali hilo kwani tayari alikuwa ameenga moyo wa kukubali
 kuwa alikuwa akiishi na virusi vya Ukimwi.

 Wito kwa jamii

 Anasema kuwa,wito wake mkubwa kwa jamii ni kuwa kuona Ukimwi kama
 ugonjwa wa kawaida na kujikubali pale unapokuwa umepata maambukizi.

“Ukimwi ni kama mafua watu wote wanakufa na makaburi yanachimbwa kila
 siku na wanaokufa na kuzikwa si wote wanaishi na virusi vya Ukimwi,
 kwani hata maralia, kisukari, kansa vyote vinaua” anasema

 Rukia anasema kuwa wenye virusi vya Ukimwi wanakupa mapema kutokana na
 upumbavu wao kwani elimu imesambaa nchi nzima namna ya kujilinda na
 hata unapokuwa umeathirika unatakiwa ufanye nini.

 Maisha yake ya sasa

 Anasema kuwa, kwa sasa maisha yake yana amani zaidi kutokana na
 kujikubali na kwa sasa anafanya kazi kama mlinzi katika Shirika la
 Tree of Hope ambao walimuwezesha kuja Dodoma kuhudhuria kongamana
 laKitaifa la wanawake.
 Anasema Tree of Hope walimpa elimu ya ukatili ili aweze kuwasaidia
 katika kufanya kazi zao.

 Pia anasema kuwa amekuwa akifanya kazi ya kutoa ushauri nasaha katika
 baadhi ya hospitali na pia mjasiriamali wa nguo.

 Rukia anasema kuwa sasa Mungu amemjalia maisha yake na amani na
 anajivunjia wajukuu 11 aliokuwa nao.


 Aidha anabainisha kuwa,aliolewa mwaka 2003 na mwanaume ambaye hana
 maambukizi ya Ukimwi na wamekuwa wakiishi pamoja moaka sasa.

 Anasema kuwa maisha yake ni ya amani na anamshukuru mumewe huyo kwa
 kumsaidia kwani mara kadhaa hulazimika kwenda kumchukulia dawa.

“Watu wengine wanasema Rukia ni muongo kaamua tu kula hela kwa
 kujitangaza kuwa na virusi” anasema

 Rukia ambaye anazifahamu ABC hazi Z za mbinu za kuepukana na Ukimwi
 anasemakubwa kuliko zote ni kuacha ngono,kubadili tabia na mapenzi si
 lazima kujamiiana.

 Anasema kuwa jamii ina nafasi nzuri za kujikinga na maambukizi ya
 Ukimwi kwani elimu imekuwa ikitolewa kila kona ya nchi cha muhimu ni
 kubadili tabia.

“Nawaambia vijana vyote ving’aavyo si dhahabu vingineni vya kuchovya
 kinga ni muhimu” anasema

 Pia anazitaja hatua nne za maambukizi kuwa ni pamoja na kipindi cha
 kwanza ni kipindi ficho ambapo unaenda kupima baada ya miezi mitatu.

 Anasema hatua ya pili unakwenda kupima lakini maambukizi hakuna wala
 huumwi na huna tatizololote.

 Hatua ya tatu ni utata mwambata huwa ni kipindi cha utatanishi unakuwa
 na magonjwa nyemelezi mara mkanda wa Jeshi, mara kifua kikuu,homa
 haziishi, majipu lakini vitu kama hivyo ukienda hospitali unapona

 Rukia anasema kuwa hatua ya nne ni kipindi tuli ukidharau  kutumia
 dawa au  kuamua kwenda kwa waganga wa kienyeji unakwenda moja kwa moja
  kwenye Ukimwi.

 Anasema kuwa ukifikia katika hatua hiyo dawa ni maombi, faraja na
 paracetamol hapo unakuwa umefika wakati wako wa kufa.
 Aidha Rukia anakumbuka mwanamke aliyemsindikiza kufaniwa kitigo
 alifariki mwaka 2000 na kitigo hicho alifanyiwa katika Kijiji cha Mtakuja.





Friday, April 18, 2014

Polisi dodoma wajipanga kudhibiti uhalifu sikukuu ya Pasaka




JESHI la Polisi Mkoani Dodoma, limesema limejipanga kuimarisha ulinzi
maeneo yote ya Mkoa wa Dodoma katika kipindi chote cha sikukuu ya
pasaka.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma Kamishna Msaidizi wa Polisi (SACP),
David Misime alisema katika kipindi cha pasaka Jeshi la polisi
limejipanga kuimarisha ulinzi maeneo yote ya mkoa wa Dodoma na
watafanya doria za miguu, pikipiki, magari na pia kutumia mbwa na
farasi.
Alisema kutokana na suala la ulinzi na usalama ni la kila mtu na wadau
mbalimbali na watashirikiana na vyombo vingine vya dola, manispaa
kampuni za ulinzi binafsi, viongozi wa serikali za mitaa na vikundi
vya ulinzi shirikishi.
“Tunachoomba ni kila mtu atambue ulinzi ni jukumu la kila moja na
unaanzia katika ngazi ya familia tunaomba waendelee kushirikiana na
Jeshi la polisi kwa kutupatia taarifa za wahalifu na uhalifu” alisema
 Alitaka kila  mtu azingatie sheria za usalama barabarani ili kuzuia
ajali,kuepuka ulevi wa kupindukia na sehemu za starehe wazingatie
sherehe.

Sunday, April 13, 2014

Ukatili wa kijinsia ulivyoharibu ndoto za Felista


Na Mwandishi wetu
UKATILI wa Kijinsia ni miongoni mwa mambo ambayo yamekuwa yakiathiri maendeleo ya wanawake. Kumekuwa na juhudi mbalimbali zinazofanywa na Serikali na Mashirika yasiyo ya Kiserikali na hata yale ya kimataifa kuhakikisha vitendo hivyo vinakomeshwa katika jamii.
Takwimu zinaonesha kuwa, ukatili wa wanawake majumbani umeendelea kuongezeka, kati ya wanawake watatu, wawili wamefanyiwa vitendo vya ukatili.
Asilimia 39 ya wanawake wenye umri kati ya miaka 15 hadi 49 wamefanyiwa vitendo vya ukatili wa kimwili na asilimia 20 ya wanawake wamewahi kufanyiwa ukatili wa kingono.
Pia takwimu zinaonesha kuwa asilimia 45 ya wanawake wamefanyiwa ukatili wa kijinsia na takribani wasichana watatu kati ya 10 wametendewa angalau tendo moja la ukatili wa kijinsia kabla ya kufikisha iaka 18.
Felister John  (30),mkazi wa Ruamlimi Wilaya ya Musoma Mkoani Mara ni miongoni mwa wanawake waliowahi kukutana na vitendo vya ukatili wa kijinsia. Mwanamke huyo ambaye sasa ni maarufu kutokana na kazi yake ya kuuuza mboga mboga anasema kuwa, aliolewa mwaka mwaka 2001 akiwa na umri wa miaka16 baada ya kumaliza elimu ya msingi.
Nilikutana na Felister wakati wa Kongamano la Kitaifa la wanawake lililoandaliwa na Muunganio wa asasi zinazoshughulikia masuala na kijinsia lililomalizika hivi karibuni mkoani Dodoma.
Licha ya ucheshi wake lakini ni mwenye historia ndefu katika maisha yake ambapo wakati mwingine unaweza kuona hailingani na umri wake.
Kulingana na Felista siku chache baada ya kufunga ndoa  wakaenda kijijini kwa mumewe Tarime  kusalimia na kufikia kwa shemeji yake ambaye ni kaka wa mume wake .
Cha ajabu shemeji yake akaanza kumtaka kimapenzi  jambo ambalo hakukubaliana nalo na huo ukawa mwanzo wa kufanyiwa visa na kuna siku aliwahi kumtamkia kuwa kuna kitu kibaya atamfanyia kwani yeye ni muolewaji tu.
Baada ya muda akaanza kuugua kichomi, ndipo shemeji yake aliposema kuwa anataka amtengenezee dawa lakini cha kushangaza dawa ilikuwa ni pilipili iliyokuwa imesagwa.
 “Shemeji aliweka mkaa kwenye sufuria , moto ulikuwa mkali, nikakalishwa chini nikaambiwa nipanue mguu wakaweka moto chini ya miguu na kisha nikafunikwa na shuka na  blanketi wakaja watu wakashikilia zile nguo nilizofunikwa ili hewa isiingie wala kutoka na akawekwa pilipili kwenye moto zile pilipili zilipokuwa zikiungua harufu ilikuwa kali nikaanza kushindwa kupumua” anasema
Anasema kuwa, alipofunuliwa nguo alizokuwa amefunikwa ambazo ni blanketi na shuka alikuwa hajiwezi kabisa na tayari alikuwa amejisaidia haja ndogo na alikaa kitandani siku tatu bila kutoka nje.
Shemeji yake akamuambia hiyo dawa inatakiwa irudiwe baada ya siku tatu,lakini alikataa kata kata.
“Kwa kweli sikukubali akaenda kunishtakiwa kwa mume wangu kuwa nilikuwa nikikataa na mume wangu akaungana na kaka yake kuwa ni lazima nitumie dawa ili nipone, niliamua kukimbia lakini mume wangu alinikimbiza  hadi kunikamata na kwa kushirikiana walifanikiwa kunifunika na kuniwekea tena ile dawa nikaanza kulia kuwa ninaungua mapaja wakasema acha niungue kwani walikuwa wakinitengeneza dawa” anasema
Baada yakuachiwa kutoka kwenye nguo alizokuwa amefunikwa mguu ulikuwa umeungua vibaya akawa na maumivu makali sana hali iliyosababisha kupoteza fahamu.
Hata hivyo baada ya fahamu kumrudia aligundua amejisaidia haja ndogo na kwa vile walikuwa wamembananisha mguu gamba la mguu wa kulia likabaki mguu wa kushoto na kufanya pale palipobanduka kuwa na kidonda kikubwa.
“Nikaugua mwezi mzima hakuna wa kunipelekahospitali,siwezi kutembea wala kunyanyuka najisaidia humo humo ndani  ikafikia hatua mguu ukanuka wakaniletea manyoya ya sungura na asali wakaniwekea kwenye mguu ulioungua wakasema hakuna kuosha mguu” anasema
Felista anasema kuwa,baada ya wiki mbili mguu ukawa umeoza anakumbukailikuwa ni Agosti 3, mwaka 2001 akawa mtu wa ndani tu manyoya ya Sungura aliyowekewa yalikuwa palepale lakini nyama za miguu zikawa zikidondoka chinikutokana na kuoza.
  “Nikafikiria nifanye nini nikapata wazo la kuandika barua ili ndugu zangu wapate taarifa, lakini nilipokuwa naandika barua shemeji akanikuta akachukua barua ile na kuichana nililia sana maana sikujua hatma yangu itakuwa nini” anasema

Hata hivyo akapata wazolingine la kumtuma kijana wa jirani kwenda stendi amtafute ndugu yake aitwaye Mashaka  ili aweze kuwapatia taarifa nyumbani na kwa bahati nzuri aliweza kuwapatia taarifa wakamtuma bibi mzaa mama akafika
Anasema kuwa,bibi yake alipofika alikuta akiwa na hali mbaya na wakati huo alikuwa na mimba ya miezi saba na baadaye ikaamuliwa apelekwe kijijini kwa mumewe  kule Matongo na baada ya kufika huko kikao kilikaa na kukubaliana apelekwe hospitali ya Bugando bili akakatwe mguu lakini hata hivyo kaka yake Wambura Mwikwabe ambaye anaishi Musoma alikataa.
“Wakanipeleka Musoma kwa kaka yangu nikaanza kuhudumiwa na hali yangu ikawa nzuri na siku ambayo uchungu uliponianza nikaenda hospitali na mama mkwe wangu lakini cha kushangaza aliniambia siumwi bali nilikuwa nimetamani vitanda vya hospitali jinsi vilivyokuwa vimetandikwa na kama nina uchungu mbona sioneshi dalili” anasema
Felista anasema kuwa,alijifungua siku hiyo hiyo yaani Oktoba 21, mwaka 2001 na kupata mtoto wa kike na mama yake mzazi alifika na kumhudumia  na baada ya kuruhusiwa kutoka hospitali akarudishwa tena nyumbani kwa mumewe huku akiendelea kuishi kwa manyanyaso ikafikia hatua anarudi nyumbani kwao na kisha kwa mumewe.
Anasema kuwa mtoto wake wa kike aliyejifungua kwa bahati mbaya  alifariki wakati akiwa na umri wa miezi tisa na alipobeba mimba nyingine kuna siku mumewe alimpiga na mimba hiyo kutoka.
Hata hivyo tayari ana watoto wengine watatu Anna mwenye umri wa miaka tisa anayesoma shule ya Msingi Nyakato akifuatiwa na Ayub na Zacharia ambao bado wako chekechea.
Felista anasema kuwa mwaka 2012 likazuka jambo jipya.dada yake alikuwa amelazwa hospitali na hilo likamlazimu kuchukua watoto wa dada yake na kuishi na pale nyumbani.
Jambo hilolikamkera mumewe ambaye aliwafukuza watoto hao wakati akiwa hospitalini akimuangalia mgonjwa.
“Baada ya kurudi sikuwakuta watoto wa dada, nilipomuuliza mume wangu aliniambia kuwa watoto wale wana baba na mama na hawahitaji nyumbani pale,nilishangaa kwa vile pale nyumbani kulikuwa na mama mkwe na watoto watano na ndugu wa mume wangu,nikamwambia kama wale umewafukuza basi  na hao wa ndugu wako nao waondoke kwani mtoa matumizi alikuwa ni mimi na siko tayari kutoa matumizi tena, ukawa ugomvi mkubwa” anasema
Anasema kuwa ugomvi huo ukaingiliwa na ndugu wa mumewe akiwemo wifi yake Sophia ambao walikaa kikao na kuamua kumfukuza
“Nilikataa kuondoka kwa vile nyumba ile nilikuwa nimejenga mimi na kiwanja ambacho tumejenga nyumba nilinunua mwenyewe kwa Shilingi 250,000  kutoka kwa Sophia “ anasema
Anasema kuwa, fedha za kiwanja alitoa na kumpa mumewe ili akalipie kiwanja hicho ambapo hata aliporudi na kuuliza kama kulikuwa na kuandikishiana kwa ajili ya ushahidi mumewe alimuambia kwa vile walikuwa ndugu hakuna sababu ya kuandikishiana.
“Baada ya kununua kiwanja hicho tulijenga nyumba ya matofali mabichi lakini ikabomoka na mvua na mara ya pili tukajenga ya tofali za kuchoma vyumba viwili na sebule.” anasema
Felista anakumbuka Julai 21, mwaka jana, mumewe alimpiga hadi kwenda kulazwa wodini kwa siku tatu na wakati akiwa hospitali wifi yake alitafuta gari na kutoa vitu vyote vya ndani na fedha taslimu Shilingi milioni 1.3 lakini hata hivyo majirani wakapinga vitu hivyo kuondoka.
“Nilipopata taarifa nikaenda nyumbani nikakuta Toyota Hiace iko nje wanapakia vyombo na vitanda,nikapiga yowe nikalala chini ili gari lisiondoke dereva alipotaka kuondoa gari  nikamwambia uniue  hapa hapa siondoki” anasema
Anasema kuwa alipata ujasiri wa kupiga simu kwenye Shirika la ABC Foundation ili kupata masaada kwani wana kitengo cha kutetea haki za wanawake na watoto na wao wakapiga simu polisi,mara polisi wakafika na kukuta baadhi ya watu wakishikiliwa na wananchi.
Miongoni waliokuwa wakishikiliwa ni Sophia, mdogo wa mume wangu aitwaye Paul pamoja na mama mkwe.
Hata hivyo  mume wa Sophia  alifanikiwa kukimbia na alipoingia chumbani alikuta fedha alizokuwa amehifadhi hazipo.
Polisi wakaamua vyombo hivyo vishushwe na watuhumiwa walifikishwa kituo cha polisi na wakafunguliwa mashaka.
Lakini watuhumiwa walikuwa wakicheleweswa kufikishwa mahakamani  lakini Agosti 3, mwaka jana walifikishwa mahakama ya mwanzo Kitaji,Musoma.
Anasema kuwa kabla ya kufikishwa mahakamani watuhumiwa hao polisi walikuwa wakimzungusha na hapo aliamua kwenda kwa Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya kuomba msaada jambo lililowachukiza askari na kusema kuwa alikuwa akiwachongea kwa bosi wao kwani walikuwa wamemuambia alete shahidi ili kesi iende Mahakama ya Wilaya.
Tangu kesi imefunguliwa mashahidi wamekuwa wakizungushwa kilawakienda kesi inaahirishwa,.
“Lakini naamini mahakama itatenda haki kwani nyumba ile ni yangu na hata fedha walizochukua naomba Mungu warudishe kwani nilikuwa nikidunduliza muda mrefu kutokana na biashara yangu ya kuuza mboga mboga” anasema
 Anasema kuwa mumewe tangu ampige na kukimbilia Tarime kwa kaka yake Julai mwaka jana, mpaka sasa bado hajarudi na amekuwa akilea watoto peke yake.
Felista anataka wanawake kuvunja ukimya pindi wanapofanyiwa mambo ya ukatili kwani ukatili umekuwa wakati mwingine ukikatisha uhai na hata kusababisha vilema vya maisha.
“Wanawake wasikae kimya wanapofanyiwa ukatili, wawe wazi ili waweze kusaidiwa,mimi naona kama nilikosea kuolewa na mwanaume yule kwani mara kadhaa nimenusurika kupoteza maisha kutokana na kipigo” anasema
Anasema kuwalicha ya kufanyiwa ukatili mara kadhaa ikiwemo kuchomwa moto, kupigwa hadi mimba kutoka na hata kutaka kudhulimiwa nyumba lakini ameendelea kufanya shughuli zake kama kawaida kutokana na kutokaa kimya kwani matukio mengi ya ukatili aliyokuwa akifanyiwa amekuwa akitoataarifa hali ambayo mara nyingi hata majirani wamekuwawakimtetea pindi wanapoona kuwa haki haikutendeka.

Mguu wa Felista unavyoonekana kwa sasa baada ya kupona


2.Felista akizungumza wakati wa kongamano la kitaifa la wanawake lililofanyika Mjini Dodoma.




Safari bado ndefu kufikia usawa wa kijinsia


Na Mwandishi Wetu
“LAZIMA wanawake wajengewe uwezo tunataka nchi inayojali usawa wa kijinsia, hatutaki kusikia maneno ya kejeli kwa wanawake wanaojitokeza kugombea uongozi kwa  lengo la kuwavunja moyo ili warudi nyuma”
Maneno hayo yanasemwa na mwanasiasa Mkongwe na Mbunge wa viti maalum Anna Abdallah wakati wa mkutano wa Umoja wa Wanawake Wanasiasa nchini (Ulingo) uliofanyika Mjini Dodoma.
Anabainisha kuna umuhimu kwa vyama vya siasa kuwa na demokrasia ya kweli kwani bila kufanya hivyo mfumo wake wa uendeshaji kamwe hauwezi kujali usawa wa kijinsia.
Kulingana na Abdallah vyama vingi vya siasa havina usawa wa kijinsia jambo ambalo linahitaji kufanyiwa kazi. Pamoja na hayo anasema  ataendelea kukemea vitendo vya kudhalilisha wanawake wanaotafuta uongozi.
Abdallah ambaye ni Mwenyekiti wa Ulingo anasema ataendelea kuwa mkali kuona wanawake wanaotafuta uongozi
wanapodhalilishwa  kwani wengi wao wamekuwa wakinyanyasika kwa kauli chafu na maneno ya kejeli kuwa hawawezi uongozi.
"  Ndani ya siasa wanawake wananyanyasika hasa pale wanapotafuta uongozi, utasikia mtu anasema wewe utamchaguaje mwanamke ambaye
anachuchumaa wakati wa kwenda haja, haya si maneno mazuri mtu wa namna hiyo anamdharau mwanamke ambaye ni sawa na mama yake mzazi " anasema

Kulingana na mwanasiasa huyo wanataka kuweka wazi kuwa mwanamke ana nafasi waheshimiwe kwani hata vijana wamekuwa na misemo ya ovyo juu ya wanawake wakati wamezaliwa na wanawake hao hao ambao wanawakosea adabu.
Anasema kuna haja ya kuwajengea uwezo wanawake waonekane wana uwezosawa na wanaume na kuondoa misemo ya ovyo.
“Tunapopata nafasi lazima tuelezane na tujengeane uwezo  wanawake wana fursa, nia na uwezo hasa pale wanapochaguliwa kuwa viongozi” anasema
Anabainisha kuwa bunge la sasa la katiba lina wajumbe zaidi ya 600 ambapo wajumbe 201  wanatoka maeneo mbalimbali na sasa kinachofanyika ni kuwajengea uwezo wanawake ili watakapokwenda kwenye kamati wapate
kuwasemea wanawake wenzao.
"Lazima tuelezane na kujengeana uwezo tunataka nchi  inayotetea usawawa kijinsa  lazima ifike wakati ionekane kila mtu ana thamani sawa" anasema
Aidha maslahi ya wanawake wa Tanzania  yanaendana na uwazi na hapendi kuona kunakuwa na udhalilishaji ua utoaji wa maneno machafu kwa wanawake wanaojitokeza kugombea nafasi mbalimbali
Mbunge wa Viti Maalum, Suzan Lyimo(Chadema) anataka wanawake walio bungeni kuwaunga mkono na kuwachagua wanawake wanaogombea nafasi mbalimbali .
Pia katika rasimu ya kwanza amani ilikuwa ni moja ya tunu ya taifa lakini katika rasimu ya pili tunu hiyo haipo na wana jukumu la kuhakikisha tunu ya amani inarudi ili kwenda sambamba na mambo mengine.
Anataka Ulingo kusimama na kukemea hasa pale ambapo wanaona mwanamke anadhalilishwa, hata anapofanyiwa hivyo na vyombo vya habari.
Aidha ,Mbunge wa viti maalum, Margareth Sitta anasema mpaka sasa Tanzania imeshindwa kurudisha shuleni wanafunzi wanaopata mimba ili waendelee na masomo pindi wanapojifungua.
"Tunapoteza wasichana wenye uwezo mkubwa, Nchini Kenya Mwanafunzi
anapojifungua anaruhusiwa kuendelea na masomo hapa Tanzania kuna nini?" anasema
Alitaka katiba iwe na kipengele cha kurudisha tena kwenye masomo
wanafunzi wanaopata ujauzito.
"Tuongeze kipengele hicho kwenye katiba hiii ili wanafunzii wanaopata
mimba waendelee na masomo.
Victoria  Lihiru kutoka Ulingo anasema  mchakato wa katiba haukusahau wanawake  kutokana na kujitokeza kwa masuala mengi ya kijinsia.
Anasema rasimu ya pili imeweka wazi kuwa wanawake wote ni sawa.
"Kwenye tunu za taifa, amani haijatajwa ,usawa wa kijinsia haujatajwa ni suala la kupigia kelele ili vitu hivyo virudi" anasema
Anabainisha kuwa haki za wanawake zipo lakini hakuna tume ya kusimamia utekelezaji wake kwani katiba ni kitu kimoja na utekelezaji ni kitu kingine.
Pia haki za wanawake wenye ulemavu pia zimekosekana kwenye
rasimu ya pili ambayo pia haijasema haijasema nani ni mtoto kama ni miaka 18 au 21 katiba ni lazima iainishe mtoto ni nani.
"Hata vyama vya siasa havijabanwa kuzingatia masuala ya kjinsia pia
katika suala la kufanya maamuzi katiba imebaki kimya.Katika nchi
nyingine  kuna bajeti katika masuala ya kijinsia yamekuwa yakitengewa bajeti na hivyo kurahisisha  utekelezaji wa vipaumbele mbalimbali.
Aidha Mjumbe wa Bunge la katiba, Dk.Ave Maria Semakafu anataka kuwe na tume ya kufuatilia masuala ya usawa wa kijinsia ambapo Stella Jairos kutoka Sauti ya Wanawake wenye ulemavu Tanzania anasema walemavu ni kundi pekee la unyonge ambalo huwezi kukwepa  ukweli uliopo.
Pia anasema elimu  ni chanzo cha maarifa yote vilevile ni chanzo cha kila jambo wanawake wenye ulemavu wafikiriwe kupewa nafasi za bure katika shule za msingi na sekondari ili kuongeza idadi ya wanawake wanaopata elimu ambayo itawasaidia katika maisha yao.
Vilevile anataka walemavu wathaminiwe katika suala la usalama wa uzazi.
Pamoja na hayo hata katika masuala ya kodi yaangaliwe kwani walemavu wasioona wamekuwa  wakiingia gharama mara mbili kutokana na kulipa watu wanaowaangoza wakati kiwango cha malipo wanayofanyia kazi yakikatwa kodi na kupungua hali inayofanya maisha kwao kuwa magumu.
Jairos anasema katika rasimu ya pili kulikuwa hakuna makala za kutosha .
“Shirika la Oxfam lilifadhili nakala 50 nchi nzima watu wengi wenye ulemavu rasimu ya pili hawaijui” anasema
Mbunge wa Kasulu Vijijini, kupitia Chama cha NCCR-Mageuzi ,Agripina Buyogera  anasema sasa wanawake wamebadilika na kuwa na mshikamano sana.
Anasema alisimama na kugombea Ubunge kupitia jimbo na alifanikiwa kuchaguliwa anaamini kama wakiingia 50/50 wanawake wanaweza.
Pia Mbunge huyo anasema sasa anasoma elimu ya sekondarii ili aweze kupata cheti cha kidato cha nne kwani wakati akichaguliwa kuwa Mbunge alikuwa na elimu ya darasa la saba na anajiendeleza ili aweze kuwa na sifa za kugombea nafasi hiyo tena.
“Kutokana na umaskini sikubahatika kupata elimu nikachaguliwa kuwa Mbunge nikiwa na elimu ya darasa la saba na sasa najiendeleza, wanawake wanaweza” anasema
Anasema vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia na udhalilishaji vimekuwa vikitokea mara kwa mara kuna wakati wanaona wanawake wananyanyaswa na kubughudhiwa wajitahidi na kujenga ushujaa wa kujiamini.
 
Mwanasiasa Mkongwe Nchini, Anna Abdalah