UKATILI wa Kijinsia ni miongoni mwa mambo ambayo
yamekuwa yakiathiri maendeleo ya wanawake. Kumekuwa na juhudi mbalimbali
zinazofanywa na Serikali na Mashirika yasiyo ya Kiserikali na hata yale ya
kimataifa kuhakikisha vitendo hivyo vinakomeshwa katika jamii.
Takwimu zinaonesha kuwa, ukatili wa wanawake
majumbani umeendelea kuongezeka, kati ya wanawake watatu, wawili wamefanyiwa
vitendo vya ukatili.
Asilimia 39 ya wanawake wenye umri kati ya miaka 15
hadi 49 wamefanyiwa vitendo vya ukatili wa kimwili na asilimia 20 ya wanawake
wamewahi kufanyiwa ukatili wa kingono.
Pia takwimu zinaonesha kuwa asilimia 45 ya wanawake
wamefanyiwa ukatili wa kijinsia na takribani wasichana watatu kati ya 10
wametendewa angalau tendo moja la ukatili wa kijinsia kabla ya kufikisha iaka
18.
Felister John
(30),mkazi wa Ruamlimi Wilaya ya Musoma Mkoani Mara ni miongoni mwa
wanawake waliowahi kukutana na vitendo vya ukatili wa kijinsia. Mwanamke huyo
ambaye sasa ni maarufu kutokana na kazi yake ya kuuuza mboga mboga anasema
kuwa, aliolewa mwaka mwaka 2001 akiwa na umri wa miaka16 baada ya kumaliza
elimu ya msingi.
Nilikutana na Felister wakati wa Kongamano la
Kitaifa la wanawake lililoandaliwa na Muunganio wa asasi zinazoshughulikia
masuala na kijinsia lililomalizika hivi karibuni mkoani Dodoma.
Licha ya ucheshi wake lakini ni mwenye historia
ndefu katika maisha yake ambapo wakati mwingine unaweza kuona hailingani na
umri wake.
Kulingana na Felista siku chache baada ya kufunga
ndoa wakaenda kijijini kwa mumewe
Tarime kusalimia na kufikia kwa shemeji
yake ambaye ni kaka wa mume wake .
Cha ajabu shemeji yake akaanza kumtaka kimapenzi jambo ambalo hakukubaliana nalo na huo ukawa
mwanzo wa kufanyiwa visa na kuna siku aliwahi kumtamkia kuwa kuna kitu kibaya atamfanyia
kwani yeye ni muolewaji tu.
Baada ya muda akaanza kuugua kichomi, ndipo shemeji
yake aliposema kuwa anataka amtengenezee dawa lakini cha kushangaza dawa
ilikuwa ni pilipili iliyokuwa imesagwa.
“Shemeji
aliweka mkaa kwenye sufuria , moto ulikuwa mkali, nikakalishwa chini nikaambiwa
nipanue mguu wakaweka moto chini ya miguu na kisha nikafunikwa na shuka na blanketi wakaja watu wakashikilia zile nguo nilizofunikwa
ili hewa isiingie wala kutoka na akawekwa pilipili kwenye moto zile pilipili zilipokuwa
zikiungua harufu ilikuwa kali nikaanza kushindwa kupumua” anasema
Anasema kuwa, alipofunuliwa nguo alizokuwa
amefunikwa ambazo ni blanketi na shuka alikuwa hajiwezi kabisa na tayari
alikuwa amejisaidia haja ndogo na alikaa kitandani siku tatu bila kutoka nje.
Shemeji yake akamuambia hiyo dawa inatakiwa irudiwe
baada ya siku tatu,lakini alikataa kata kata.
“Kwa kweli sikukubali akaenda kunishtakiwa kwa mume
wangu kuwa nilikuwa nikikataa na mume wangu akaungana na kaka yake kuwa ni
lazima nitumie dawa ili nipone, niliamua kukimbia lakini mume wangu
alinikimbiza hadi kunikamata na kwa
kushirikiana walifanikiwa kunifunika na kuniwekea tena ile dawa nikaanza kulia
kuwa ninaungua mapaja wakasema acha niungue kwani walikuwa wakinitengeneza
dawa” anasema
Baada yakuachiwa kutoka kwenye nguo alizokuwa
amefunikwa mguu ulikuwa umeungua vibaya akawa na maumivu makali sana hali
iliyosababisha kupoteza fahamu.
Hata hivyo baada ya fahamu kumrudia aligundua
amejisaidia haja ndogo na kwa vile walikuwa wamembananisha mguu gamba la mguu
wa kulia likabaki mguu wa kushoto na kufanya pale palipobanduka kuwa na kidonda
kikubwa.
“Nikaugua mwezi mzima hakuna wa
kunipelekahospitali,siwezi kutembea wala kunyanyuka najisaidia humo humo
ndani ikafikia hatua mguu ukanuka
wakaniletea manyoya ya sungura na asali wakaniwekea kwenye mguu ulioungua
wakasema hakuna kuosha mguu” anasema
Felista anasema kuwa,baada ya wiki mbili mguu ukawa
umeoza anakumbukailikuwa ni Agosti 3, mwaka 2001 akawa mtu wa ndani tu manyoya
ya Sungura aliyowekewa yalikuwa palepale lakini nyama za miguu zikawa
zikidondoka chinikutokana na kuoza.
“Nikafikiria
nifanye nini nikapata wazo la kuandika barua ili ndugu zangu wapate taarifa,
lakini nilipokuwa naandika barua shemeji akanikuta akachukua barua ile na
kuichana nililia sana maana sikujua hatma yangu itakuwa nini” anasema
Hata hivyo akapata wazolingine la kumtuma kijana wa
jirani kwenda stendi amtafute ndugu yake aitwaye Mashaka ili aweze kuwapatia taarifa nyumbani na kwa bahati
nzuri aliweza kuwapatia taarifa wakamtuma bibi mzaa mama akafika
Anasema kuwa,bibi yake alipofika alikuta akiwa na
hali mbaya na wakati huo alikuwa na mimba ya miezi saba na baadaye ikaamuliwa
apelekwe kijijini kwa mumewe kule Matongo
na baada ya kufika huko kikao kilikaa na kukubaliana apelekwe hospitali ya
Bugando bili akakatwe mguu lakini hata hivyo kaka yake Wambura Mwikwabe ambaye
anaishi Musoma alikataa.
“Wakanipeleka Musoma kwa kaka yangu nikaanza
kuhudumiwa na hali yangu ikawa nzuri na siku ambayo uchungu uliponianza nikaenda
hospitali na mama mkwe wangu lakini cha kushangaza aliniambia siumwi bali
nilikuwa nimetamani vitanda vya hospitali jinsi vilivyokuwa vimetandikwa na
kama nina uchungu mbona sioneshi dalili” anasema
Felista anasema kuwa,alijifungua siku hiyo hiyo
yaani Oktoba 21, mwaka 2001 na kupata mtoto wa kike na mama yake mzazi alifika
na kumhudumia na baada ya kuruhusiwa
kutoka hospitali akarudishwa tena nyumbani kwa mumewe huku akiendelea kuishi
kwa manyanyaso ikafikia hatua anarudi nyumbani kwao na kisha kwa mumewe.
Anasema kuwa mtoto wake wa kike aliyejifungua kwa
bahati mbaya alifariki wakati akiwa na
umri wa miezi tisa na alipobeba mimba nyingine kuna siku mumewe alimpiga na
mimba hiyo kutoka.
Hata hivyo tayari ana watoto wengine watatu Anna
mwenye umri wa miaka tisa anayesoma shule ya Msingi Nyakato akifuatiwa na Ayub
na Zacharia ambao bado wako chekechea.
Felista anasema kuwa mwaka 2012 likazuka jambo
jipya.dada yake alikuwa amelazwa hospitali na hilo likamlazimu kuchukua watoto
wa dada yake na kuishi na pale nyumbani.
Jambo hilolikamkera mumewe ambaye aliwafukuza watoto
hao wakati akiwa hospitalini akimuangalia mgonjwa.
“Baada ya kurudi sikuwakuta watoto wa dada, nilipomuuliza
mume wangu aliniambia kuwa watoto wale wana baba na mama na hawahitaji nyumbani
pale,nilishangaa kwa vile pale nyumbani kulikuwa na mama mkwe na watoto watano
na ndugu wa mume wangu,nikamwambia kama wale umewafukuza basi na hao wa ndugu wako nao waondoke kwani mtoa
matumizi alikuwa ni mimi na siko tayari kutoa matumizi tena, ukawa ugomvi
mkubwa” anasema
Anasema kuwa ugomvi huo ukaingiliwa na ndugu wa
mumewe akiwemo wifi yake Sophia ambao walikaa kikao na kuamua kumfukuza
“Nilikataa kuondoka kwa vile nyumba ile nilikuwa
nimejenga mimi na kiwanja ambacho tumejenga nyumba nilinunua mwenyewe kwa
Shilingi 250,000 kutoka kwa Sophia “ anasema
Anasema kuwa, fedha za kiwanja alitoa na kumpa
mumewe ili akalipie kiwanja hicho ambapo hata aliporudi na kuuliza kama
kulikuwa na kuandikishiana kwa ajili ya ushahidi mumewe alimuambia kwa vile
walikuwa ndugu hakuna sababu ya kuandikishiana.
“Baada ya kununua kiwanja hicho tulijenga nyumba ya
matofali mabichi lakini ikabomoka na mvua na mara ya pili tukajenga ya tofali
za kuchoma vyumba viwili na sebule.” anasema
Felista anakumbuka Julai 21, mwaka jana, mumewe
alimpiga hadi kwenda kulazwa wodini kwa siku tatu na wakati akiwa hospitali
wifi yake alitafuta gari na kutoa vitu vyote vya ndani na fedha taslimu
Shilingi milioni 1.3 lakini hata hivyo majirani wakapinga vitu hivyo kuondoka.
“Nilipopata taarifa nikaenda nyumbani nikakuta
Toyota Hiace iko nje wanapakia vyombo na vitanda,nikapiga yowe nikalala chini
ili gari lisiondoke dereva alipotaka kuondoa gari nikamwambia uniue hapa hapa siondoki” anasema
Anasema kuwa alipata ujasiri wa kupiga simu kwenye Shirika
la ABC Foundation ili kupata masaada kwani wana kitengo cha kutetea haki za
wanawake na watoto na wao wakapiga simu polisi,mara polisi wakafika na kukuta
baadhi ya watu wakishikiliwa na wananchi.
Miongoni waliokuwa wakishikiliwa ni Sophia, mdogo wa
mume wangu aitwaye Paul pamoja na mama mkwe.
Hata hivyo mume wa Sophia
alifanikiwa kukimbia na alipoingia chumbani alikuta fedha alizokuwa
amehifadhi hazipo.
Polisi wakaamua vyombo hivyo vishushwe na watuhumiwa
walifikishwa kituo cha polisi na wakafunguliwa mashaka.
Lakini watuhumiwa walikuwa wakicheleweswa kufikishwa
mahakamani lakini Agosti 3, mwaka jana
walifikishwa mahakama ya mwanzo Kitaji,Musoma.
Anasema kuwa kabla ya kufikishwa mahakamani
watuhumiwa hao polisi walikuwa wakimzungusha na hapo aliamua kwenda kwa Mkuu wa
Upelelezi wa Wilaya kuomba msaada jambo lililowachukiza askari na kusema kuwa
alikuwa akiwachongea kwa bosi wao kwani walikuwa wamemuambia alete shahidi ili
kesi iende Mahakama ya Wilaya.
Tangu kesi imefunguliwa mashahidi wamekuwa
wakizungushwa kilawakienda kesi inaahirishwa,.
“Lakini naamini mahakama itatenda haki kwani nyumba
ile ni yangu na hata fedha walizochukua naomba Mungu warudishe kwani nilikuwa
nikidunduliza muda mrefu kutokana na biashara yangu ya kuuza mboga mboga”
anasema
Anasema kuwa
mumewe tangu ampige na kukimbilia Tarime kwa kaka yake Julai mwaka jana, mpaka
sasa bado hajarudi na amekuwa akilea watoto peke yake.
Felista anataka wanawake kuvunja ukimya pindi
wanapofanyiwa mambo ya ukatili kwani ukatili umekuwa wakati mwingine ukikatisha
uhai na hata kusababisha vilema vya maisha.
“Wanawake wasikae kimya wanapofanyiwa ukatili, wawe
wazi ili waweze kusaidiwa,mimi naona kama nilikosea kuolewa na mwanaume yule
kwani mara kadhaa nimenusurika kupoteza maisha kutokana na kipigo” anasema
Anasema kuwalicha ya kufanyiwa ukatili mara kadhaa
ikiwemo kuchomwa moto, kupigwa hadi mimba kutoka na hata kutaka kudhulimiwa
nyumba lakini ameendelea kufanya shughuli zake kama kawaida kutokana na kutokaa
kimya kwani matukio mengi ya ukatili aliyokuwa akifanyiwa amekuwa akitoataarifa
hali ambayo mara nyingi hata majirani wamekuwawakimtetea pindi wanapoona kuwa
haki haikutendeka.
![]() |
Mguu wa Felista unavyoonekana kwa sasa baada ya
kupona
|
![]() |
2.Felista akizungumza wakati wa kongamano la kitaifa
la wanawake lililofanyika Mjini Dodoma.
|


No comments:
Post a Comment