Tuesday, April 22, 2014

Mila ya kuondoa mikosi 'kitigo' ilivyomsababishia Ukimwi

“NILIPATA maambukizi ya Ukimwi mwaka 1990, nakumbuka baada ya kifo cha  mume wangu niliambiwa nirithiwe na mdogo wa mume jambo hilo nililipinga , nduguze wakasema kama sitaki kuolewa lazima uondoe kitigo (mkosi) bila hivyo utaua ukoo mzima huo ukawa ni mwanzo wa safari ndefu katika maisha yangu kwani baada ya muda mfupi nilianza
 kudhoofika na baadaye kugundulika ninaishi na VVU”

Maneno hayo yanasemwa na Rukia Issa Majata (59) mkazi wa Sahare Tanga.

 Nilimfahamu mwanamke huyu wakati wa kongamano la wanawake Kitaifa
 lililofanyika Mkoani Dodoma.Hata nilipomuomba kwa ajili ya kufanya
 naye mahojiano hakuwa na shaka.

“Mimi niko tayari wakati wowote na niko tayari kueleza kitu gani
 kimenitokea katika maisha yangu ili jamii izidi kuongeza juhudi
 kupinga mila potofu wanazofanyiwa wanawake na wakati mwingine zimekuwa
 zikigharimu maisha yao” anasema mama huyo.

 Akiwa ni mwanaharakati wa masuala ya Ukimwi na hata nyanja za ukatili
 wa kijinsia anasema kuwa, aliolewa mwaka 1972 na Denea Mwendo ambaye
 kwa sasa ni marehemu.

 Anasema kuwa,mume wake alifariki mwaka 1990 na wakati huo tayari
 alikuwa na watoto wanane.

 Hata hivyo,anasema kuwa,baada ya msiba huo kuisha wana ukoo walikaa na
 kuamua aridhiwe na mdogo wa mume wake jambo ambalo hakukubaliana nalo
 lakini wakasema kama hataki kurithiwa ni lazima aondoe kitigo (mkosi)
 la sivyo atamaliza ukoo mzima.

 Anasema kuwa  aliambiwa hayo kabla hata hajamaliza eda, japo alikuwa
 akikataa lakini alikuwa hana sauti kutokana na wao kuwa wengi na
 alitakiwa kutafutwa mwanaume aliyefiwa na mume ambaye alikuwa
 hamfahamu

 Ndipo ulipofika usiku akasindikizwa na mwanamke moja ambaye hamfahamu
 kwa jina na yule bwana wa kwenda kumuondoa kitigo alisindikizwa na
 mwanaume mwenzake na walipofika huko wakafanya tendo la ndoa huku wote
 wakiwa hawajuani,  wakati huo ilikuwa ni saa nne za usiku kwa hiyo
 ilikuwa si rahisi kumtambua mtu kutokana na giza lililokuwepo.

 Rukia anasema kuwa, baada ya miezi sita  akaona afya yake inashuka na
 wakati huo ilikuwa ni mwishoni mwa mwaka 1990 ,akaona ni heri akapate
 ushauri wa kupima virusi vya Ukimwi.

 Baada ya kupima akagundulika kuwa ana maambukizi ya Virusi vya Ukimwi
 hali ambayo ilimchanganya lakini akaamua kumshukuru Mungu kwa kila
 jambo.

 Hata hivyo alipewa rufaa ya kwenda hospitali ya Bombo kwa ajili ya
 kupima ini, wingi wa damu na CD4 na baada ya wiki moja alifuatilia
 majibu  na kuonekana kuwa alikuwa na CD4 1050 jambo ambalo lilifanye
 asianze kutumia dawa.

‘Nilipewa mlolongowa chakula ambachokitanisaidia na mambo ambayo
 yatafanya nisishushe kinga yangu”anasema

 Anasema kuwa mwanaume aliyemfanyia kitigo ndiye atakuwa amemuambukiza
 Ukimwi kwani hata marehemu mume wake hakuwahi kuugua ugonjwa huo na
 alianza kudhoofika muda mfupi baada ya kubakwa na mwanaume aliyetakiwa
 kumuondoa mkosi.

 Japokuwa aliamua kumuachia Mungu juu ya maisha yake na kuamua kuishia
 kwa masharti aliyokuwa akielekezwa na masdaktari hali ambayo imemfanya
 kuwa na afya njema mpaka sasa.

 Hata hivyo anasema kuwa, mwaka 2006 alifiwa na binti yake  aliyemtaja
 kwa jina la Rehema na hapo kinga yake ya mwili ikashuka kutokana na
 mshtuko ambao ulifanya ashindwe kula na wakati huo ndiyo alianza
 kutumia dawa za kupunguza makali ya Ukimwi (ARV).

 Anasema kuwa tangu wakati huo ameendelea kutumia ARV lakini mpaka sasa
 CD4 zake ziko1066.

 Siri ya mafanikio

 Rukia anasema kuwa,ameamua kuwa kioo cha jamii na amekuwa akielimisha
 vijana mashuleni na sehemu mbalimbali ikiwemo kwenye mikutano, warsha
 na makongamano endapo atachaguliwa kwani amekuwa hana wasiwasi kabisa.

“Mwaka 1999  nilijitangaza kuwa ninaishi na virusi vya Ukimwi  hiyo ni
 baada ya kujiunga na Umoja la watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi Mkoa
 wa Tanga TAPHA+  na baada ya kujitangaza baadhi ya watu waliamini na
 wengine hawakuamini lakini nilikuwa nimeondoa mnyororo wa wasiwasi”
anasema

 Anasema baada ya kujitangaza kuna watu walikuwa wakimnyooshea vidole
 lakini hakujali hilo kwani tayari alikuwa ameenga moyo wa kukubali
 kuwa alikuwa akiishi na virusi vya Ukimwi.

 Wito kwa jamii

 Anasema kuwa,wito wake mkubwa kwa jamii ni kuwa kuona Ukimwi kama
 ugonjwa wa kawaida na kujikubali pale unapokuwa umepata maambukizi.

“Ukimwi ni kama mafua watu wote wanakufa na makaburi yanachimbwa kila
 siku na wanaokufa na kuzikwa si wote wanaishi na virusi vya Ukimwi,
 kwani hata maralia, kisukari, kansa vyote vinaua” anasema

 Rukia anasema kuwa wenye virusi vya Ukimwi wanakupa mapema kutokana na
 upumbavu wao kwani elimu imesambaa nchi nzima namna ya kujilinda na
 hata unapokuwa umeathirika unatakiwa ufanye nini.

 Maisha yake ya sasa

 Anasema kuwa, kwa sasa maisha yake yana amani zaidi kutokana na
 kujikubali na kwa sasa anafanya kazi kama mlinzi katika Shirika la
 Tree of Hope ambao walimuwezesha kuja Dodoma kuhudhuria kongamana
 laKitaifa la wanawake.
 Anasema Tree of Hope walimpa elimu ya ukatili ili aweze kuwasaidia
 katika kufanya kazi zao.

 Pia anasema kuwa amekuwa akifanya kazi ya kutoa ushauri nasaha katika
 baadhi ya hospitali na pia mjasiriamali wa nguo.

 Rukia anasema kuwa sasa Mungu amemjalia maisha yake na amani na
 anajivunjia wajukuu 11 aliokuwa nao.


 Aidha anabainisha kuwa,aliolewa mwaka 2003 na mwanaume ambaye hana
 maambukizi ya Ukimwi na wamekuwa wakiishi pamoja moaka sasa.

 Anasema kuwa maisha yake ni ya amani na anamshukuru mumewe huyo kwa
 kumsaidia kwani mara kadhaa hulazimika kwenda kumchukulia dawa.

“Watu wengine wanasema Rukia ni muongo kaamua tu kula hela kwa
 kujitangaza kuwa na virusi” anasema

 Rukia ambaye anazifahamu ABC hazi Z za mbinu za kuepukana na Ukimwi
 anasemakubwa kuliko zote ni kuacha ngono,kubadili tabia na mapenzi si
 lazima kujamiiana.

 Anasema kuwa jamii ina nafasi nzuri za kujikinga na maambukizi ya
 Ukimwi kwani elimu imekuwa ikitolewa kila kona ya nchi cha muhimu ni
 kubadili tabia.

“Nawaambia vijana vyote ving’aavyo si dhahabu vingineni vya kuchovya
 kinga ni muhimu” anasema

 Pia anazitaja hatua nne za maambukizi kuwa ni pamoja na kipindi cha
 kwanza ni kipindi ficho ambapo unaenda kupima baada ya miezi mitatu.

 Anasema hatua ya pili unakwenda kupima lakini maambukizi hakuna wala
 huumwi na huna tatizololote.

 Hatua ya tatu ni utata mwambata huwa ni kipindi cha utatanishi unakuwa
 na magonjwa nyemelezi mara mkanda wa Jeshi, mara kifua kikuu,homa
 haziishi, majipu lakini vitu kama hivyo ukienda hospitali unapona

 Rukia anasema kuwa hatua ya nne ni kipindi tuli ukidharau  kutumia
 dawa au  kuamua kwenda kwa waganga wa kienyeji unakwenda moja kwa moja
  kwenye Ukimwi.

 Anasema kuwa ukifikia katika hatua hiyo dawa ni maombi, faraja na
 paracetamol hapo unakuwa umefika wakati wako wa kufa.
 Aidha Rukia anakumbuka mwanamke aliyemsindikiza kufaniwa kitigo
 alifariki mwaka 2000 na kitigo hicho alifanyiwa katika Kijiji cha Mtakuja.





No comments:

Post a Comment