Wednesday, August 5, 2015

Mpwapwa yageuka jangwa

WILAYA ya Mpwapwa iko katika hatari ya kugeuka jangwa kutokana na wananchi kukosa mbinu za kilimo chenye kuhifadhi mazingira.

Kauli hiyo imetolewa na  maofisa wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Msanga Mabusi na Paskali Mpemba wakati wakizungumza  katika maohojiano maalumu.

Maofisa hao wakizungumza kwa pamoja wamesema kwamba kukosekana kwa wataalamu wa kutosha wa ugani kushawishi kilimo chenye tija na maslahi kwa mazingira kumefanya wakulima kukata miti hovyo.

Walisema ni jukumu la wananchi kuona namna bora ya kufanya kilimo kwa kuwa wanayahitaji maizngira hayo ili kuwa na maisha nendelevu katika kilimo na ustawi wa jamii husika.

Mabusi amesema kumekuwepo na uharibifu mkubwa wa mazingira katika
wilaya ya Mpwapwa kunakotokana na wananchi wananchi kukosa  elimu ya mbinu bora za kilimo na kutokuwa na mpango wa matumizi bora ya ardhi.

Alisema wananchi wamekuwa wakikata miti hovyo kwa ajili ya kuandaa mashamba mapya na hivyo kutishia wilaya hiyo kugeuka jangwa kutokana na kilimo cha kuhamahama wakitafuta maeneo yenye rutuba.

Aidha amesema pamoja na jitihada za serikali na kuwapo kwa sheria
ya misitu namba 14 ya mwaka  2002  bado tatizo la uharibifu wa
misitu limekuwa ni kubwa na hivyo kuhatarisha usalama wa maisha ya binadamu pamoja na wanyama .

Kwa upande wake  Paskal Mpemba  alisema kuwa kama viongozi kuanzia
ngazi ya vitongoji ,vijiji na kata  na idara tofauti hawataunganisha nguvu  kulikabili uharibifu wa mazingira basi madhara yake yatakuwa makubwa na kugusa jamii nzima na kuifanya Mpwapwa kuendelea kuwa duni.
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kwamba kila kijiji kina kamati ya mazingira, lakini badala ya kukabiliana na waharibifu , nyingi ya kamati hizo zinafumbia macho kinachoendelea kutokea cha uharibifu wa mazingira kwa kukatwa hovyo kwa miti.

No comments:

Post a Comment