KUISHI na wake wengi si kazi rahisi na sasa sina nguvu
nazeeka, sitaoa tena wanawake nilionao wanatosha”.
![]() |
| Nzije Shanga Komite |
Maneno hayo yanasemwa na mfugaji wa kabila la Kimasai, Nzije
Shanga Komite mkazi wa Kijiji cha Mkakatika Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma
ambaye ana wake 12 na watoto 52. Alipoulizwa na mwandishi wa makala haya idadi
ya watoto aliyonayo alisema hafahamu lakini mtoto mkubwa wa mzee huyo anasema
wako watoto 52 katika familia hiyo wakiwemo wa kike 30 na wa kiume 22.
“Nina wake 12, watoto wengi wengi hata majina siwakumbuki na
wengine wamepata wenzao wanajitegemea,” anasema mzee huyo. Mfugaji huyo ambaye
amepanga ratiba ya kulala na kila mke wake, anasema kuishi na wake wengi si
rahisi kwani kuna wakati huwa anachoka na kutaka kupumzika.
Mzee huyo akiwa ni kati ya wafugaji 68 wa Wilaya ya Bahi
walioamua kubadilika na kuvuna mifugo yao ili kuwa na maisha ya kisasa. Kwa
mujibu wa Mzee huyo anasema alizaliwa mwaka 1955 kijijini hapo ambapo wazazi
wake walikuwa wafugaji na hakupata muda wa kwenda shule kutokana na kufanya
kazi ya kuchunga mifugo ya baba yake ambapo maisha yao yalikuwa ya kuhamahama
kutafuta malisho.
Mzee Nzije anasema mke wake wa kwanza alimuoa mwaka 1979.
Mwanamke huyo ambaye alifanikiwa kuzaa naye watoto sita alifariki mwaka jana na
kuzikwa kwenye boma la nyumba yake. Mtoto wake wa kwanza alizaliwa mwaka 1984
na tangu wakati huo amekuwa akioa mfululizo, wakati mwingine wake wawili au
watatu kwa mwaka moja hadi walipofikia wake 12.
Pia mke wa mwisho alimuoa mwaka 2007 ambaye anaitwa Gasi na
wanaishi wote mpaka leo, lakini hajafanikiwa kupata mtoto. Amekuwa akiwahudumia
wanawake hao kwa mavazi, malazi, chakula na matibabu pindi wanapougua.
Anakumbuka mkewe wa kwanza ambaye kwa sasa ni marehemu alimuoa kwa mahari ya
ng’ombe 27 na mkewe wa mwisho alimuoa kwa mahari ya ng’ombe 12.
Amekuwa akiwapangia zamu wanawake hao kwa ajili ya kulala nao
ambapo kwa mwanamke moja amekuwa akikaa kwa siku tatu au nne kisha kwenda kwa
mwanamke mwingine. “Kuna wakati huwa nachoka na huwa nawaambia sitaki kabisa
nimechoka siwezi kufanya kitu,” anasema.
Anaona kadiri siku zinavyokwenda anazidi kuwa na umri mkubwa
na hivyo si rahisi tena kushiriki mapenzi na wake zake kila mara. Hata hivyo,
kulingana na mila za Kimasai mwanamke anapokuwa na ujauzito hadi kujifungua
anatakiwa kukaa miaka miwili bila kukutana na mwanamume. “Hata unapokwenda
kumgusa anakataa anasema anaweza kuharibu mtoto wake,” anasema.
Alipoulizwa amekuwa akifuata njia za uzazi wa mpango alisema,
wake zake hawatumii njia za uzazi wa mpango bali wamekuwa wakifuata mila zao
kwa kusubiri miaka miwili tangu ajifungue na hata baada ya mtoto kuacha
kunyonya ndipo anaweza kukutana na mumewe.
“Hawatumii uzazi wa mpango wanarekebisha wenyewe huwa wanajua
siku zao za hatari hata akipata ujauzito anakaa mpaka ajifungue na anakuwa
mpweke kwa miaka miwili hadi akimwachisha mtoto kunyonya hapo anaruhusiwa
kuendelea na tendo la ndoa,” anasema.
Akielezea manufaa aliyopata tangu aanze kuvuna mifugo ni
pamoja na kununua gari la kutembelea, kujenga nyumba ya kulala wageni Bahi
Mjini, kununua trekta la kisasa na pia ameweza kununua kiwanja Bahi Mjini
ambapo anatarajia kujenga nyumba ya kisasa ambayo ataishi na familia yake.
Hata hivyo anasema ukame umekuwa na athari kubwa kwa mifugo
yake kutokana na mwaka jana ng’ombe wake 1,800 kufa kutokana na ukame wa
kutisha ulioikumba Wilaya ya Bahi. Mbali na hayo anasema amenunua trekta ili
aendeshe kilimo cha kisasa ambapo mwaka huu anatarajia kulima ekari 70 za
mahindi, mtama na ufuta.
![]() |
| sehemu ya familia |
Aidha, maji kwa ajili ya kunywesha mifugo yamekuwa tabu,
lakini wanahangaika kwa kuhamisha hamisha mifugo ambapo sasa ana ng’ombe
wanaokaribia 1,000 ambao amewagawa katika makundi. Mzee huyo, hivi karibuni
alikabidhiwa ramani ya nyumba na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma kwa ajili ya ujenzi wa
makazi bora kutokana na kuhamasika na kuamua kuuza baadhi ya mifugo yake ili
aweze kujenga makazi bora.
Lakini bado hajaanza ujenzi huo kutokana kutafuta fedha za
kumaliza kulipa mkopo wa trekta ambapo sasa anadaiwa Sh milioni 27. Pia alikopa
trekta hilo pamoja na jembe lake ambapo trekta pekee lilikuwa likiuzwa kwa Sh
milioni 32 na ameshalipa milioni 11. Mbali na hilo Mzee huyo amechangia fedha
kwa ajili ya ujenzi wa Shule ya Msingi Kidete.
Kulingana na mzee huyo changamoto kubwa ni uhaba wa maji,
lakini anafanya juhudi kuhakikisha anatafuta wataalamu ili aweze kuchimba
kisima. Pamoja na hayo anachotamani sasa ni kuchimba kisima ambacho kitaondoa
adha ya upatikanaji wa maji katika familia yake na hata kwa ajili ya kunywesha
idadi kubwa ya mifugo aliyonayo.
Anabainisha kuwa amebadili mawazo na sasa nyumba ya kisasa
anayotaka kuijenga kijijini Mkakatika sasa ataijenga Bahi Mjini baada ya
kununua kiwanja kikubwa. Nyumba ya kisasa anayotaka kuijenga itakuwa na vyumba
nane na sebule ambapo anataka iwe nyumba bora ya mfano kwa wafugaji wengine.
Aidha anachosubiri ni kupata hati, kuchora ramani ili ujenzi
uanze, lakini anategemea kuanza baada ya msimu wa kilimo kwani anatarajia mazao
atakayopata akiuza fedha zitakazopatikana ndizo zitumike kwa ajili ya ujenzi wa
nyumba. Mmoja wa wake wa mzee huyo, Eva Ishando (29) anasema ni mke wa mzee
huyo, lakini hakumbuki aliolewa akiwa mke wa ngapi ila anachokumbuka aliolewa
mwaka 2004.
Mama huyo mwenye watoto watatu anasema mtoto wa kwanza na wa
pili alijifungulia katika Kituo cha Afya cha Bahi, lakini mtoto wa tatu
alijifungulia nyumbani kutokana na kupata uchungu akiwa bado nyumbani.
“Nilichelewa na muda ulifika nikiwa nyumbani wenzangu walinisaidia
nikajifungua,” anasema.
Umbali uliopo kijijini wanapoishi hadi hospitali imekuwa
changamoto kubwa kwani hata mtoto anapozaliwa kufuatilia chanjo za kliniki
imekuwa ni kazi ngumu. Pia anaitaja changamoto nyingine ni upatikanaji wa maji
ambapo wamekuwa wakichota maji umbali wa kilomita 20 kutoka wanapoishi kwenye
Kijiji cha Ugimaa.
“Shule, hospitali na hata tunakochota maji ni mbali, maji
tumekuwa tukichota kwa kutumia punda,” anasema. Mke mwingine wa mzee huyo ni
Gaudencia Nzije (45) ambaye ana watoto saba. Anasema maisha ya kijijini si
rahisi kwani huduma muhimu zimekuwa zikipatikana umbali mrefu, lakini hata
hivyo pindi wanapougua mumewe hutafuta usafiri kwa ajili ya kuwafikisha
hospitali.
Kwa upande wake, Kezia Nzije akiwa kati ya wake wa mzee huyo
ambaye kwa umri anaonekana mdogo anasema hakumbuki alizaliwa mwaka gani, lakini
amezaa na mzee huyo mtoto moja ambaye kwa sasa ana umri wa miezi saba, anataja
jina la mtoto huyo kuwa ni Kilaita. “Mtoto huyu nilimzaa Mei mwaka huu na
nilijifungulia nyumbani,” anasema.
![]() |
| sehemu ya familia |
Mmoja wa watoto wa mzee huyo Mafanya Nzije (12), anayesoma
darasa la pili katika Shule ya Msingi Lowassa kijijini hapo anasema anaona
maisha ya nyumbani hapo ni ya kawaida kwani amekuwa akihudhuria shule na
anataka kusoma hadi amalize darasa la saba.
Kwa upande wake mzee huyo ambaye ni mmoja wa wafugaji 68 wa
Wilaya ya Bahi walioamua kubadilika ili waweze kuishi maisha ya kisasa kwa
kuvuna mifugo yao, anasema hakubahatika kupata elimu na alipokuwa mdogo alikuwa
akichunga mifugo ya baba yake jambo lililofanya kukosa fursa ya kupata elimu.
Anasema anafurahia maisha anayoishi baada ya kuamua kubadilika
ambapo aliuza baadhi ya mifugo yake na kununua gari kwa ajili ya kutembelea na
sasa amefungua nyumba ya kulala wageni ambayo pia ina biashara ya baa Bahi
Mjini. Mkuu wa Wilaya ya Bahi, Betty Mkwasa anasema sasa amejizatiti kuhakikisha
wanafikia wafugaji wengi ili wapate elimu na hatimaye kuvuna mifugo ili waweze
kuwa na makazi bora.
Alisema katika wilaya hiyo kuna wafugaji wenye ng’ombe wengi
wanaoishi maisha yasiyo bora wakati wanaweza kupunguza mifugo hiyo kwa kuuza na
kupata fedha za ujenzi wa makazi bora na hata kupeleka watoto wao shuleni.
Anasema katika mpango huo wa kuhamasisha wafugaji kuwa na makazi bora
wamefanikiwa kwani mzee huyo sasa ameweza kujenga nyumba ya kulala wageni
ambayo pia imetoa ajira wa wananchi wengine.
![]() |
| Akiwa na mkuu wa mkoa |
![]() |
| Mkuu wa mkoa Dk Nchimbi akionesha ramani ya makazi ya Mzee |
Mkwasa anasema waliamua kumtengenezea mzee huyo ramani kwa
ajili ya kuboresha makazi yake kutokana na kuwa ni mkulima na mfugaji mkubwa,
lakini anaishi kwenye nyumba ya tembe. Mkwasa anasema mzee huyo pia
alihamasishwa kuingia katika kilimo bora na cha kisasa na sasa amefanikiwa
kununua trekta ambalo litamsaidia katika shughuli mbalimbali.
“Mzee Nzije ni mpenda maendeleo najitahidi kumbadilisha awe
mfugaji wa mfano yaani kufuga kisasa na kilimo ndiyo maana nilimsimamia
akopeshwe trekta,” anasema Mkwasa. Anasema anataka mfugaji huyo awe mfano
katika elimu hasa kusomesha watoto wake vizuri ili wafike mbali.
Imetoka kwa mara ya kwanza Nyota habarileoJumapili

















